Pages

Thursday, March 3, 2016

DIWANI WA CCM AUMBULIWA MBELE YA MBUNGE, WANANCHI WAMZOMEA WAGOMEA MAAMUZI YAKE

Diwani wa kata ya Ng'ang'ange wilaya ya Kilolo Bw Namgalesi Lusumsuva akisisitiza jambo baada ya  kutoa maamuzi magumu ya kuteua majina  mawili ya mabinti ambao watakaimu nafasi ya afisa mtendaji wa kijiji cha Ng'ang'ange kabla ya wananchi kumpinga, kulia ni Mbunge wa jimbo la Kilolo Venance Mwamoto.

Mbunge Mwamoto akimpatia namba ya simu mmoja kati ya wasanii kijiji  cha Ng'ang'ange anayeomba kufika kuwa mgeni rasmi katika uzinduzi wa albamu yake.
DIWANI  wa kata ya Ng'ang'ange  wilaya ya  kilolo mkoani Iringa Bw Namgales  Msuva (CCM) amejikuta katika  wakati mgumu  mbele ya  mbunge wa  jimbo la Kilolo Bw Venance Mwamoto baada wananchi  kumzomea kama  njia  ya  kupinga uteuzi  wake  usio  shirikishi wa makaimu wawili    watendaji wa  kata  ya Ng'ang'ange .

Wananchi hao    walifikia hatua   hiyo jana  wakati wa mkutano wa hadhara  wa mbunge  wao kuwashukuru  kwa  kumchagua  kuwa mbunge  wao katika  uchaguzi mkuu uliofanyika mwaka jana .

Kabla  ya  diwani   huyo  kupingwa mbele ya  wananchi na mbunge  kuingilia kati kutuliza jazba  za  wananchi hao ,alikuwa  amewateua wasichana  wawili wakazi wa kijiji  cha Ng'ang'ange  akiwemo Felista Ngogo ambae alikuwa akikaimu nafasi hiyo na msaidizi  wake Flora Magoda  kuendelea  kukaimu nafasi hiyo .

Kwani  diwani   huyo alisema  kuwa  sababu ya  yeye  kufanya uteuzi huo ni  baada ya awali  kuteua  mtendaji wa muda ambae aliacha nafasi hiyo  baada ya  wananchi  kuonyesha  kumpuuza katika maagizo  mbali mbali aliyoyatoa.

Hivyo  alisema haiwezekani ofisi  hiyo  kukosa afisa mtendaji  wa kata kwa  zaidi ya miezi 6  hivi  sasa na yeye akiwa kama mwenyekiti wa kamati ya maendeleo ya kata  hiyo na diwani ameamua kufanya uteuzi wa maofisa hao  watendaji wawili badala ya mmoja ili  kuifanya kazi   hiyo.

" Mtendaji  katika  ofisi hii ya kata hayupo na  ofisi  imekuwa  ikifungwa muda  wote .....utendaji kata  si ajira halipwi chochote  sasa  mimi kama  diwani na mwenyekiti wa kata  natumia nafasi yangu kuwateua mabinti hawa  wawili ambao wataifanya kazi hii ya  kujitolea  kuanzia  leo nimeona  tunalala  sana .....natoa amri kuanzia  sasa mnanisikiliza " alisisitiza diwani  huyo

Huku  akitaka wananchi  ambao  wanatuhumiwa kwa ushirikina na pamoja na  vijana  wanaoshinda  vijiweni kufikishwa mbele ya  ofisi  yake ya kata  haraka   ili  kuchapwa  viboko.

Hatua   hiyo  ya  uteuzi wa maofisa  watendaji hao ilipelekea  mkutano  huo wa mbunge  kuvurugika kwa muda baada ya  wananchi hao kupinga ubabe wa diwani  wao  huyo kwa kufanya uteuzi pasipo kushirikisha baraza la  maendeleo ya  kata wala wahusika   wenyewe  kushirikishwa .

Wananchi hao  walisema  hawautambui uteuzi  wa maofisa  hao wa kata na  kuwa hao  aliowateua ni maofisa wa nyumbani kwake na  sio katika ofisi  hizo za serikali ngazi ya kata .

Mbali ya  wananchi  kuzomea  na  kumkataa diwani  huyo kwa maamuzi yake pia mabinti  hao  walijitokeza hadharani na  kukataa uteuzi huo kuwa hauna maslahi kwao na  wao  hawajashirikishwa kabla ya  kutangazwa hivyo hawapo tayari  kufanya kazi   hiyo kutokana  na  diwani  kutowashirikisha mapema .

Mbunge wa Kilolo Bw Mwamoto  alilazimika  kusimama na kusitisha uteuzi  huo kufuatia  maombi ya  wananchi  kumtaka  kuingilia kati maamuzi ya  diwani  huyo ambayo hayakushirikisha  kiongozi wala  mjumbe mwingine  yeyote  wa ngazi ya  kijiji  wala kata.

Bw  Mwamoto  alisema anasitisha  uteuzi huo  wa diwani  kwa  watendaji hao na  yeye kama  mbunge atawasiliana na ofisi ya mkurugenzi  mtendaji wa Halmashauri  ya  wilaya ya  Kilolo ili baada ya ajira  mpya  za  watendaji kutolewa basi kata  hiyo kupewa  kipaumbele na  kwa  sasa wakati  zoezi hilo  bado  kufanyika mwenyekiti wa  serikali ya kijiji  cha Ng'ang'ange ataendelea kukaimu nafasi ya utendaji  wa kata  pia.

Maamuzi hayo ya mbunge  Mwamoto  alionyesha  kuwafurahisha  wananchi  hao  wakiwemo wale wa upinzani  kutoka chama cha Demokrasia na maendeleo (Chadema ) ambao  walimpongeza mbunge kwea  busara  zake na  kuahidi  kuendelea  kutoa ushirikiano kwa mbunge   huyo na mwenyekiti  aliyeteuliwa kukaimu  utendaji wa kata.

Mbunge  wa  Kilolo Bw Venance Mwamoto wa kwanza  kulia akicheza ngoma ya njuga na  wasanii wa asili kijiji  cha Ng'ang'ange baada ya  kufika katika  mkutano wa hadhara.

No comments: